Usafi wa moyo (kwa Kiingereza: chastity, kutoka Kilatini: castitas) ni neno lilivyotumiwa na Yesu katika Hotuba ya mlimani kwa maana pana kabisa na inayohusisha unyofu wa dhamiri kwa jumla.
Hata hivyo, neno hilo linatumika mara nyingi, hasa katika Kanisa Katoliki[1][2][3], kuelezea adili ambalo linapingana na uzinifu na kutegemea kiasi na ambalo linasisitizwa sana na Biblia na Kurani. Kwa maana hiyo unawahusu watu wanaojua kutawala maelekeo ya kijinsia yaweze kujenga maisha yao binafsi, familia na hata jamii.
Hapa tutazingatia usafi wa moyo kama aina muhimu zaidi ya adili la kiasi, kwanza kwa jumla, unavyotakiwa katika hali yoyote ya maisha, hata katika ndoa. Halafu tutaona unavyozaa Kiroho, hasa ukitekelezwa kwa namna bora, yaani katika ubikira. Juu yake, Yesu alisema, “Awezaye kulipokea neno hili, na alipokee” (Math 19:12). Mtaguso wa Trento umetamka rasmi kwamba hali ya useja mtakatifu ni bora kuliko ile ya ndoa, kama Mtume Paulo alivyofundisha wazi katika Waraka wa kwanza kwa Wakorintho 7:25,38,40.