Muziki wa Tanzania | |
---|---|
Asili ya utamaduni | Tanzania |
Inapotendeka | |
Dar es Salaam |
Muziki wa Tanzania ni muziki wenye asili yake katika eneo la Tanzania ya leo. Kama ilivyokuwa kwa binadamu wengine, wakazi wa eneo hilo, walikuwa na utamaduni wao. Utamaduni huo ulikuwa ukitofautiana kati ya kabila na kabila. Moja ya vipengele ilikuwa muziki. Kiasili, hakukuwa na ‘muziki’ katika makabila hayo kabla ya ujio wa wageni, hivyo hakuna kabila lenye tafsiri ya neno muziki.
Lakini watu waliimba, walicheza ngoma, walipiga vyombo mbalimbali, ila walikuwa na utamaduni mwingine kuhusu kitu hiki tunachokiita siku hizi muziki. Watafiti wanatuambia tulikuwa na ngoma, ambayo tafsiri yake ni kubwa kuliko muziki.
Ngoma ilikuwa chombo kile kilichotoa muziki, ngoma ilikuwa shughuli yenyewe, kwa mfano ngoma ya mavuno, ngoma ya mashetani na kadhalika, na pia watu walicheza ngoma. Pamoja na kukosekana kwa maandiko yenye kina kuhusu hali ya ngoma katika kipindi hicho lakini tunajua watu waliimba na kucheza ngoma kwa matukio mbalimbali, hali ambayo inaendelea mpaka leo.